ULIMWENGU WA KIISILAMU

ULIMWENGU WA KIISLAMU, FURSA NA CHANGAMOTO


Assalamu alaikum ndugu Waislamu
hichi ni kijitabu kilichokusanya idadi ya makala kutoka Radio ya kiswahili ya Iran (kiswahili.irib.ir), na mkusanyaji wa makala hizi ni ndugu yenu Salim Al-Rajihiy, kwa hiyo haki za kunukuu au kuchapisha zimehifadhiwa na (kiswahili.irib.ir) Iran, na hakukua na malengo yeyote katika kuzikusanya makala hizi, isipokua ni kueneza fikra na utamaduni wa Kiislamu. Ahsanteni sana tusiache kuombeana dua.


Ulimwengu wa Kiislamu Fursa na Changamoto
Kwa jina Allah Mwingi wa rehema Mwenye Kurehemu Assalaam Alaykum wasomaji na wapenzi wa Redio Tehran Idhaa ya Kiswahili Sauti ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Huu ni mfululizo wa makala za Ulimwengu wa Kiislamu, Fursa na Changamoto ambao utatupia jicho na kuchunguza fursa pamoja na changamoto zinazoukabili Ulimwengu wa Kiislamu. Ulimwengu wa Kiislamu si jina geni katika fasihi, maandiko, istilahi za kisiasa na kiutamaduni na hata katika masikio ya walimwengu pia.


Kabla ya neno Ulimwengu wa Kiislamu kubainisha hali ya eneo fulani kijiografia, linabeba maana na kuweka wazi utambulisho wa jamii fulani ya watu wapatao bilioni moja na nusu ambao wana mitazamo, dini, utamaduni,ustaarabu, mila na desturi zinazoshabihiana. Mbali na sifa maalumu ulionao ulimwengu wa Kiislamu kijiografia, ulimwengu huu una maliasili na utajiri mkubwa, utajiri ambao umeufanya kufahamika kuwa, eneo lenye utajiri mkubwa kabisa duniani. Sifa hiyo na suhula ulizonazo ndiyo zilizoufanya ulimwengu wa Kiislamu kwa karne kadhaa kuwa na nafasi muhimu katika uhusiano wa kimataifa. Hapana shaka kuwa, pana haja ya kuainishwa malengo na mipango madhubuti ambayo itasaidia kustafidi vizuri na suhula hizo na kwa njia sahihi na iliyo bora.


Katika mfululizo huu wa ''Ulimwengu wa Kiislamu, Fursa na Changamoto'' tutazungumza na kujadili fursa na suhula zilizopo katika nchi za Kiislamu ambazo bila shaka kutumiwa kwake vyema kutaimarisha nafasi ya Waislamu katika nyanja mbali mbali ulimwenguni iwe ni kiuchumi au kisiasa na vile vile kuyaleta na kuyakurubisha pamoja mataifa ya Kiislamu na wafuasi wa dini hii tukufu. Aidha tutatupia jicho pia changamoto zinazoukabili ulimwengu wa Kiislamu zikiwemo za kiutamaduni, kiuchumi, kisiasa, kielimu na kadhalika.

Matukio ya hivi sasa ulimwenguni yamebainisha kwamba, madola ya kibeberu hayataki kuona ulimwengu wa Kiislamu ukiwa na nafasi muhimu katika matukio mbalimbali duniani. Madola yanayopenda kujitanua daima yanatafakari na kutaamali ni namna gani yataweza kuudhibiti ulimwengu wa Kiislamu. Ndio maana madola hayo yakawa hayako tayari kuukubali utamaduni asili na tajiri wa Kiislamu, hasa kutokana na kuwa, utamaduni huo si tegemezi wala hauigi tamaduni za mataifa au watu wengine. Masuala hayo na mengineyo, ndiyo yaliyoufanya Ulimwengu wa Kiislamu leo hii ukabiliwe na vitisho na migogoro ya kupandikizwa kuliko karne za nyuma; na hapana shaka kuwa, yote hayo yanatokana na njama za maadui wa Uislamu.


Ili ulimwengu wa Kiislamu uinue nafasi na kiwango chake pamoja na kudiriki utambulisho wake halisi, pana haja ya kuweko mitazamo mipya, mwamko, kuwa macho pamoja na mipango imara na madhubuti. Ili tuwe na taswira ya mustakbali wa huko tuelekeako, kuna haja ya ulimwengu wa Kiislamu kufahamu nafasi yake halisi ya hivi sasa, suala ambalo litasaidia mno kufikiwa malengo muhimu na aali na yenye mafanikio makubwa. Kama tulivyoashiria mwanzoni mwa makala hii Ulimwengu wa Kiislamu ni jina ililopewa jamii ya Waislamu yenye idadi ya takribani watu bilioni moja na nusu ambao wanapatikana na kuishi katika nchi za Kiislamu na zisizo za Kiislamu.


Kinachoifungamanisha pamoja jamii hiyo licha ya kuwa na makabila, lugha na rangi tofauti ni dini tukufu ya Kiislamu. Bara la Asia ndilo linaloongoza kwa kuwa na Waislamu wengi ambao idadi yao inakadiriwa kufikia bilioni moja. Barani Afrika kuna Waislamu wapatao milioni 391. Amma katika bara la Ulaya takwimu zinaonyesha kwamba, kuna Waislamu wapatao milioni 20 na wengine zaidi ya milioni 27 wanapatikana nchini Russia. Kadhalika kuna idadi nyingine ya Waislamu takribani milioni tisa huko Amerika ya Latini, Marekani na Canada.


Kuna baadhi ya mataifa na lugha ambazo zina nafasi muhimu katika ulimwengu wa Kiislamu. Kwa mfano lugha za Kiarabu, Kifarsi na Kituruki zinahesabiwa kuwa lugha muhimu mno katika ulimwengu wa Kiislamu. Waaidha Waislamu wengi wanaopatikana katika nchi za Pakistan na India wanazungumza lugha ya Ki-Urdu. Karibu asilimia 14 ya idadi ya Waislamu katika Ulimwengu wa Kislamu wanapatikana katika nchi za Indonesia na Malaysia na wanazungumza lugha ya Kimalayu au Kimalay.


Moja kati ya maeneo ya kiistratejia katika ulimwengu wa Kiislamu, ni eneo la Mashariki ya Kati ambayo ni njia fupi zaidi ambayo inayaunganisha mabara ya Asia na Ulaya. Lango bahari na vivuko muhimu vya kiistratejia kama vile Kanali ya Suez, Malango Bahari ya Jabal Twariq na Hormoz ni baadhi ya njia muhimu za mawasiliano ya baharini baina ya mabara mbalimbali, ambazo zinapatikana katika ulimwengu wa Kiislamu. Kuweko maliasili, nishati na utajiri wa madini na bidhaa mbalimbali za mazao ni baadhi tu ya mambo yanayouongezea umuhimu Ulimwengu wa Kiislamu na kuufanya uzingatiwe mno kimataifa.



Kama inavyofahamika, mataifa ya Kiislamu yanaundwa na lugha na makabila mbalimbali. Katika nchi 19 za Kiislamu, asilimia kubwa ya wakazi wake ni Waarabu na Wasemiti. Hata hivyo, kuna watu wengine wa makabila ya wachache kama vile Waturuki katika nchi za Kiarabu kama vile Iraq na Syria. Katika nchi za Kiafrika ambazo wakazi wake ni Waarabu wanapatikana pia watu wa jamii ya Wabarbari.


Ulimwengu wa Kiislamu una jumla ya nchi 57 na nchi yenye wakazi wengi zaidi ni Indonesia na ile yenye wakazi wachache ni Maldives. Mbali na Afghanistan, Iraq na Palestina nchi zote za Kiislamu zimejikomboa kutoka katika makucha ya wakoloni na wavamizi. Mpenzi msomaji sina shaka utakuwa umefahamu japo kwa mukhtasari, jiografia ya kimakazi na kisiasa ya ulimwengu wa Kiislamu. Makala zetu zitakazofuata zitazungumzia kwa urefu nafasi ya nchi za Kiislamu katika masuala mbalimbali ulimwenguni

No comments:

Post a Comment

add your comment here